Share this Post

dailyvideo

KISWAHILI KUWA LUGHA RASMI EAC


Imeandikwa na Mwandishi Wetu


Katibu Mkuu wa EAC, Balozi Liberat Mfumukeko
UONGOZI wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) umesema, kuna mipango ya kukifanya Kiswahili iwe lugha rasmi ya jumuia hiyo yenye watu zaidi milioni 150.
Katibu Mkuu wa EAC, Balozi Liberat Mfumukeko ameyasema hayo wakati alipokuwa anazungumza na Balozi mpya wa Uganda nchini Tanzania, Richard Kabonero kwenye ofisi za makao makuu jijini Arusha hivi karibuni. Hadi sasa Kiswahili ni lugha ya Taifa nchini Tanzania na baadhi ya wananchi kwenye nchi nyingine wanachama wanaizungumza lugha hiyo.
Hivi karibuni Naibu Waziri Mkuu wa Uganda anayeshughulikia masuala ya EAC, Kirunda Kivejinja alisisitiza umuhimu wa wananchi kwenye nchi wanachama kukitumia Kiswahili kuwaunganisha. Kiongozi huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri EAC alisema, nchi wanachama wa EAC hazitafanikiwa kutekeleza kifungu cha 137 (2) cha makubaliano ya kuanzishwa jumuia hiyo kama hazitakitumia Kiswahili kuwaunganisha.
Aliyasema hayo Zanzibar wakati wa hafla ya kufungwa kwa Mkutano wa kwanza wa Kimataifa ulioandaliwa na Tume ya Kiswahili ya Afrika Mashariki (EAKC). Alisema ni muhimu kwa Kiswahili kifanywe rahisi na sehemu kubwa ya watu kwenye eneo la EAC waitumie lugha hiyo na lugha zao za asili zikiwemo za zaidi ya makabila 120 nchini Tanzania. Alitoa pendekezo kwa EAKC kutoa mapendekezo kwamba Kiswahili kitumike vipi ili kufanikiwa katika utekelezaji wa Malengo Endelevu ya Maendeleo (SDGs).
Katibu Mkuu wa EAKC, Profesa Kenneth Simala alisema kwenye mkutano huo kuwa, tume hiyo inafanya kazi kwa karibu na vyama vya Kiswahili kwenye nchi wanachama ili viwe na umoja. Wajumbe wa mkutano huo walijadili, pamoja na mambo mengine namna Kiswahili kinavyoweza kutumika kuzidisha mtangamano EAC sanjari na kuchangia utekelezaji wa malengo endelevu.
Wajumbe walieleza umuhimu wa kuanzishwa haraka mabaraza ya Kiswahili na vyama vya lugha hiyo kwenye kila nchi, kutumia lugha hiyo kwenye ngazi mbalimbali za elimu, kuhamasisha tafiti za Kiswahili na nchi wanachama kuitumia lugha hiyo kwenye programu za elimu ya watu wazima.
Wakati wa mazungumzo na Balozi Kabonero jijini Arusha, Balozi Mfumukeko alisema, pamoja na suala hilo la lugha ya Kiswahili, EAC pia inajielekeza kwenye kuongeza uwekezaji kwenye viwanda na sekta ya kilimo ikiwa ni sehemu ya mikakati kupunguza ukubwa wa tatizo la ukosefu wa ajira. Alisema, licha ya kutekeleza protokali za ushuru wa pamoja wa forodha, soko la pamoja na fedha ya pamoja, jumuiya pia inatafuta rasilimali ili kutekeleza miradi ya maendeleo ya miundombinu zikiwemo reli na barabara.
CHANZO HABARI LEO

Posted by Editor on 12:13. Filed under , . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0

0 comments for KISWAHILI KUWA LUGHA RASMI EAC

Post a Comment

Recent Entries

Recent Comments

Photo Gallery