MAAUMUZI YA MUSEVENI,KAGAME NA UHURU.
Kutoka kushoto ni Rais Paul Kagame wa Rwanda, Rais Yoweri Museveni wa Uganda na Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta. Picha ya Maktaba.
Wiki iliyopita Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, Rais wa Uganda, Yoweri
Museveni na Rais wa Rwanda, Paul Kagame walikutana Mombasa nchini Kenya
na kuzindua mradi mkubwa wa ujenzi wa reli.
Katika uzinduzi huo marais hao wameweka muda wa kuanza kwa miradi mitatu
mikubwa. Mosi kuanza kwa mradi wa ujenzi wa reli kutoka Mombasa-Kampala
mpaka Kigali, ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Eldoret-Kampala mpaka
Kigali na kujenga miundombinu ya umeme wa uhakika.
Pia wamewaagiza mawaziri wa fedha wa nchi hizo kuandaa mapendekezo ya
utekelezaji wa miradi hiyo mitatu na taarifa ya mapendekezo hayo
wanatakiwa kuitoa kwa marais hao katika mkutano ujao.
Wanazungumza lugha moja
Kwa mujibu wa mratibu wa miradi hiyo, Monique Mukaruliza, ujenzi wa
bomba la kusafisha mafuta kutoka Eldoret-Kampala mpaka Kigali,
unatarajiwa kukamilika 2017 huku kabla ya mwisho mwa mwaka huu,
viongozi wa nchi hizo wamekubaliana kuzindua ushuru wa pamoja wa
forodha kwa ajili ya kusafirisha bidhaa kwa masharti nafuu kutoka nchi
moja hadi nyingine.
Wakati hayo yakiendelea, taarifa zinaeleza kwamba ujenzi wa reli hiyo
utagharimu Dola 3.5 bilioni, lakini taarifa nyingine zinasema kwamba
mradi huo una thamani ya Dola 13 bilioni na mradi huo utakamilika mwaka
2018 huku ujenzi wa awali wa mradi wa reli kutoka Mombasa mpaka jijini
Nairobi unatarajiwa kuanza Novemba, mwaka huu.
Vilevile kuanzia Januari mwakani, Rais wa Kenya, Kenyatta na Kagame
wamekubaliana kwamba wananchi wao waanze kutumia vitambulisho vya uraia
kusafiria katika nchi hizo wakati Uganda itatumia kadi ya kupiga kura
kusafiri Kenya na Rwanda.
Mbali na hayo taarifa iliyotolewa hivi karibuni imebainisha kwamba
katika mkutano wa pili uliofanyika Mombasa wiki iliyopita, marais hao
waliwaagiza mawaziri wa fedha wa nchi hizo kuandaa mapandekezo ya
utekelezaji wa miradi hiyo ndani ya mwezi mmoja na nusu ujao.
Wataalamu wa masuala ya uchumi, wanabainisha kwamba reli hiyo itakuwa na
uwezo wa kubeba mizigo na kwenda kilometa 80 kwa saa wakati itakapoanza
kusafirisha mizigo katika ukanda huo.
Bandari ya Mombasa, inategemewa kwa zaidi ya asilimia 50 na Rwanda
katika kuagiza mizigo huku ikitegemewa na Uganda, Mashariki mwa
Demokrasia ya Kongo (DRC), Burundi, Kaskazini mwa mikoa ya Tanzania na
Sudani Kusini.
Burundi na Sudani Kusini
Katika mkutano huo marasi wa nchi hizo tatu walikubali kuijumuisha
Burundi na Sudani Kusini katika miradi hiyo baada ya kuhudhuria mkutano
huo kama wageni waalikwa.
Kutokana na makubaliano hayo ni dhahiri kwamba nchi hizo tano
zimekubaliana kufanya kazi pamoja katika utekelezaji wa miradi hiyo kwa
lengo la kuboresha maisha ya wananchi wa nchi hizo kiuchumi.
“Wawakilishi wa Burundi na Sudani Kusini wanapaswa kuwa sehemu ya miradi
hiyo na hasa katika kamati za ufundi,” inaeleza sehemu taarifa ya
mkutano huo.
Mukaruliza anabainisha kwamba Burundi na Sudani Kusini walialikwa kwenye
mkutano huo kama watamazaji na baadaye waliomba kuwa sehemu ya
kuanzisha miradi hiyo.
Katika mkutano huo Rais Kenyatta alitoa taarifa ya maendeleo ya miradi
hiyo baada ya mkutano uliofanyika Entebbe, Juni mwaka huu.
“Ninayo furaha kutoa taarifa ya mradi wa bomba la mafuta na katika
hatua ya kwanza ya maendeleo ya mradi wa bomba la mafuta, unaendelea
vizuri na hatua ya awali tayari imeanza na upembuzi yakinifu
umekamilika,” anasema Rais Kenyatta.
Pia Kenyatta anasema kuna changamoto zinazokabili nchi hizo na kwamba
wanapaswa kuungana pamoja kwa ajili ya kuzitatua na kufikia malengo
yaliyokusudiwa.
Kuhusu hati za kuruhusu watu wa Jumuia ya Afrika Mashariki kuingia
katika nchi moja hadi nyingine, katika mkutano huo suala hilo
lilijadiliwa na mawaziri husika waliagizwa kutoa taarifa kwa nchi ya
Kenya, Rwanda na Uganda katika mkutano wa tatu utakaofanyika Oktoba
mwaka huu ili mpango huo uanze Januari mosi, mwakani.
Vilevile mawaziri husika wameagizwa kukamilisha mchakato wa kutumia
vitambulisho vya uraia kabla ya Oktoba, mwaka huu ili vitumike kama hati
rasmi kusafiria katika nchi hizo Januari mosi, mwaka huu.
Katika mkutano huo, Rais wa Sudani Kusini, Salva Kiir Mayardit
aliwakilishwa na waziri wake wa masuala nje Dk Barnaba Marial Benjamin
wakati waziri wa usafirishaji wa Burundi, Deogratias Rurimunzu
alimwakilisha Rais Pierre Nkurunziza.
Mkutano mwingine utafanyika Oktoba mwaka huu jijini Kigali.
Tanzania
Mwishoni mwa Mei, Rais Jakaya Kikwete alipofanya ziara nchini Japan
aliiomba nchi hiyo kuangalia uwezekano wa kugharimia ujenzi wa reli mpya
kutoka Tanzania kwenda nchi za Rwanda, Burundi mpaka Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ombi ambalo Serikali ya nchi hiyo
ilikubali.
Rais Kikwete anasema ujenzi wa reli hiyo utarahisisha usafirishaji wa
mizigo wa nchi hizo ambazo zinaitegemea bandari ya Dar es Salaam
kusafirishia bidhaa zake.
Taarifa zinasema Kampuni ya Burlington Northern Santa Fe Railway ya
Marekani ndiyo itakayofanya ukarabati huo ambao utahusisha ujenzi wa
reli mpya kutoka Isaka hadi Kigali ambayo pia itaunganisha Jiji la
Bujumbura, Burundi.
Hata hivyo uzinduzi wa mradi wa reli ya Mombasa-Kigali, huku Rwanda na
Uganda zikitishia kujitoa kutumia bandari ya Dar es Salaam unaacha
maswali mengi.
Mwananchi
Posted by Editor
on 20:12.
Filed under
eastafricannews,
feature
.
You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0