Share this Post

dailyvideo

MADAKTARY 146 WAMETIMULIWA KISA MGOMO


MADAKTARI 146 wamefukuzwa katika hospitali mbalimbali nchini kutokana na kushiriki mgomo unaoendelea nchi nzima kwa lengo la kuishinikiza Serikali kutekeleza madai yao.

Uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa, madaktari hao walitimuliwa katika Hospitali za Bugando na Sekou Toure mkoani Mwanza na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya na ile ya Rufaa Dodoma.

Wakati Serikali ikichukua hatua hiyo, mgomo huo jana uliendelea katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Ocean Road, Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) za jijini Dar es Salaam, Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na Hospitali ya Rufaa ya KCMC mkoani Kilimanjaro.

Katika kile kinachoonekana kuwaunga mkono wenzao, madaktari bingwa wa MOI, MNH na Ocean Road jijini Dar es Salaam, jana walitangaza rasmi kuingia kwenye mgomo huo hadi madai hayo yatekelezwe.

Madai ya madaktari ni hali bora ya mazingira ya utoaji huduma nchini, ongezeko la mishahara, posho za kufanya kazi katika mazingira magumu, posho za kufanya kazi katika mazingira hatarishi na posho za kuitwa kazini.

Tamko la madaktari hao bingwa, lilitolewa jana na msemaji wao, Dk Catherine Mng'ong'o muda mfupi baada ya kumalizika kwa kikao chao kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Tamko hilo limekuja siku moja baada ya baadhi yao kuanza kushiriki mgomo huo juzi, kushinikiza pamoja na mambo mengine, Serikali itoe tamko juu ya tukio la kutekwa na kujeruhiwa kwa Dk Ulimboka.

Hata hivyo, wakati madaktari hao wakitoa tamko hilo, uongozi wa Moi jana ulitoa tangazo kuwataka madaktari wote walioshiriki mgomo huo kurejea kazini ifikapo Julai 2, mwaka huu, vinginevyo watafukuzwa kazi.

Jana jengo la MOI lilikuwa limefungwa kwa makufuli, huku wagonjwa wakielezwa kuwa huduma zote hazitolewi zikiwamo za dharura ambazo awali ziliendelea kutolewa.
Mmoja wa walinzi aliwambia waandishi wa habari kuwa, amefunga mageti kutokana na amri ya mkuu wake wa kazi.
“Mimi ninatekeleza amri ya bosi wangu, amenitaka kufunga geti na hakuna mtu kuingia, awe mgonjwa au ninyi waandishi wa habari kwa kuwa hakuna huduma zinazotolewa humu,” alisema.
Mkoani Mwanza
Madaktari 63 walio katika mafunzo ya vitendo kazini wa Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Hospitali ya Mkoa Sekou Toure wametimuliwa na kurejeshwa wizarani kutokana na mgomo huo.

Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Dk Charles Majinge alisema kuwa, juzi aliwataka madaktari waliokuwa katika mgomo kurejea kazini, lakini hawakufanya hivyo na jana akaamua kuwarejesha 47 wizarani.

Katika Hospitali hiyo ya Mkoa wa Mwanza Sekou Toure, Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk Valentino Bangi alisema, madaktari 16 wamesimamishwa kufanya kazi kutokana na agizo la wizara.
Chanzo: Vijimambo Blog

Posted by Editor on 14:18. Filed under , . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0

0 comments for MADAKTARY 146 WAMETIMULIWA KISA MGOMO

Post a Comment

Recent Entries

Recent Comments

Photo Gallery