Share this Post

dailyvideo

HAWA NDIO WANAWAKE VIJANA 10 KUTOKA TANZANIA WALIOONESHA NJIA. WASOME HAPA





 

SUSAN MASHIBE

Ni mwanamke jasiri, mpiganaji mwenye utaalam wa masuala ya anga aliyethibitishwa na Mamlaka ya Anga Marekani (FAA). Anamiliki Kampuni ya TanJet inayojihusisha na utoaji wa ushauri wa masuala ya anga ndani na nje ya nchi.
Mwaka jana, alinukiwa Tuzo ya Kiongozi Kijana Ulimwenguni (Global Young Leader), aliyopewa na Jukwaa la Uchumi Duniani (WEF). Kampuni yake imekuwa ikipata tenda mbalimbali barani Afrika, Ulaya, Marekani na kadhalika. Jopo la wajumbe wa Baraza la Congress nchini Marekani, lilipotembelea Tanzania mwaka 2009, Mashibe ndiye aliyeratibu masuala ya anga kuhusu ujio wao.
 

FLAVIANA MATATA

Mwaka 2007 alipokwenda kushiriki mashindano ya dunia ya Miss Universe na kushika nafasi ya sita, wengi walidhani huo ndiyo mwisho wake. Ilionekana hivyo kwa sababu warembo wengi wameshiriki mashindano ya dunia na baada ya kurudi nchini, hawakusikika tena.
Kwa Flaviana, huo ulikuwa ni mwanzo wa kupiga hatua zaidi kusaka mafanikio yake. Hivi sasa, mrembo huyo ni mwanamitindo wa kimataifa, anayefanya kazi na makampuni makubwa ulimwenguni.
 

HAPPINESS MAGESSE

Miss Tanzania aliyechukua taji hilo mwaka 2001, Happiness Magesse ndiye aliyefanikiwa zaidi kimataifa kuliko wote, japo wapo wengine wanaojitahidi. Hivi sasa Happiness ‘Millen’ ni mwanamitindo wa kimataifa.
 

EMELDA MWAMANGA

Ni mwanzilishi aliye pia Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Relim Entertainment inayomiliki jarida maarufu la Kiingereza, Bang. Jinsi alivyoweza kulisimamisha jarida hilo na kulifanya kuwa maarufu zaidi nchini, inatosha kumpongeza kwamba ameonesha njia.
 

LADY JAYDEE

Jina lake asilia ni Judith Wambura. Ni mwanamuziki wa kike mwenye mafanikio zaidi ambayo chanzo chake ni muziki. Anamiliki bendi na mgahawa wa kisasa ambao ulimgharimu zaidi ya shilingi milioni 100 kuuanzisha. Bila shaka Jaydee ameonesha njia kwa wanamuziki wengine wa kike hapa nchini.
 

MADAM RITA

Kuanzisha kitu wakati mwingine inaweza kuwa jambo rahisi lakini uimara wa mtu ni pale anapoweza kulisimamia na kufanikiwa. Rita Paulsen anastahili pongezi kwa namna alivyoweza kuanzisha Shindano la Bongo Star Search na kulifikisha hapa lilipo. Huyu ni mwanamke kijana aliyeonesha njia ya kweli ya mafanikio.
 

RAHMA AL-KHAROOS

Anamiliki Kampuni ya RBP Oil & Industrial Technology. Uwezo wake uliweza kuwashtua wengi pale alipoweza kujitolea mamilioni ya fedha kuiwezesha Timu ya Taifa ya Wanawake, Twiga Stars. Mwanamke huyu ni mfano tosha kwamba inawezekana kama tu utaamua kupambana.
 

SHEAR NASSA

Anamiliki maduka ya Shear Illusions, vilevile ana jarida linaloitwa Shear Hair & Beauty. Ukubwa wa maduka yake, heshima na umaarufu wake kwa uuzaji wa vitu vya urembo ni kielelezo cha kumthibitisha Shear kwamba ni mwanamke kijana aliyefanikiwa, kwa hiyo ameonesha njia.
 

KHADIJA MWANAMBOKA

Mbunifu wa mavazi wa kike mwenye umaarufu kuliko wanawake wote nchini. Ameanza harakati zake akiwa na umri mdogo na kwa alipofikia hivi sasa, ameshaonesha njia kwa wanawake wengine nchini. Jambo muhimu ni kusimamia fani yako mpaka kuifikisha kwenye kiwango bora. Khadija alipofikia kwa ubunifu wa mavazi, anastahili pongezi.
 

FINA MANGO

Alipata umaarufu mkubwa kwenye fani ya utangazaji wa redio lakini alipoamua kuanzisha kampuni yake ya One Plus, ameweza kupata mafanikio makubwa. Tenda ya kuratibu na kusimamia Tuzo za Muziki Tanzania (Tuzo za Kili) kwa miaka mitatu mfululizo imedhihirisha ubora wa kampuni yake.


***************************************************


         
UPO msemo uliotawala vichwa vya watu tangu dahari kwamba wanawake ni tabaka la kukaa nyumbani na kufanya kazi za ndani. Wao jukumu lao ni kumfurahisha mume na lingine ni kuwaandaa watoto kwa ajili ya kwenda shule na kufuatilia nyenendo zao darasani.

Ilivyozoeleka ni kwamba wanawake ni goigoi. Utaona bungeni kuna wabunge wa viti maalum ambavyo wengi hutafsiri kuwa ni vya upendeleo. Kwa maana kwamba uwezo wao kushindana kwenye majimbo na kushinda ni mdogo ndiyo maana wanapewa hivyo maalum kwao.


Katika mitihani, kuna unafuu wa alama za ufaulu kwa wanafunzi wa kike. Yaani wanaonekana hawana uwezo wa kushindana na wavulana. Vijijini, wanawake wamekuwa wakitumika kama nyenzo ya kilimo, yaani mama akalime ndiyo alishe familia, baba akacheze bao au kunywa pombe.


Miaka inakwenda, wapo wanawake wengi ambao wameweza kudhihirisha kwamba inawezekana kwa jinsi ya kike kuanzisha kazi na kufanikiwa. Aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha-Rose Migiro ni mfano wenye nguvu kwa wanawake kufanikiwa.


Spika wa Bunge, Anne Makinda, Mchungaji Getrude Rwakatare na wengineo, ni kichocheo kinachotoa uthibitisho kuwa wanawake wanaweza. Ni suala la kuwaamini na kuwapa nafasi, kwa hakika wanaweza kufanya mambo makubwa mno.

Ukiachana na hao, ipo orodha ya wanawake vijana 10 ambao wanastahili pongezi. Wamepambana katika maeneo yao kiasi cha kupata mafanikio ambayo yameonesha njia. Inabidi tuwatambue na kuthamini jitihada zao kwa maana wameendelea kuthibitisha ndivyo sivyo kwa wale waliokuwa wanaamini kuwa wanawake si lolote kwenye utafutaji.

Chanzo: Uwazi.

Posted by Editor on 12:38. Filed under , , . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0

1 comments for HAWA NDIO WANAWAKE VIJANA 10 KUTOKA TANZANIA WALIOONESHA NJIA. WASOME HAPA

  1. Anonymous

    huyo no moja ndio kiboko

Post a Comment

Recent Entries

Recent Comments

Photo Gallery