Share this Post

dailyvideo

MWALIMU WA RAIS KAGAME MSINGI BADO ASHIKA CHAKI

Imeandikwa na KIGALI, Rwanda
“UKIWA mwalimu, hakika wewe ni mtu muhimu sana katika malezi ya mwanafunzi, kwani una nafasi kubwa ya kupenda mapema na kujifunza kutoka kwako kwa sababu wewe ni mwalimu, mlezi na kioo cha mwanafunzi, haya yakiunganishwa yanaweza kumtengeneza mwanafunzi bora,” anaandika Kahlil Gibran katika kitabu chake, The Prophet `Mtume’, akioanisha majukumu aliyonayo mwalimu.
Walimu kwa upande wao, wanasema zawadi kubwa kwao ni kuona wanafunzi wao wanakuwa na mafanikio katika jamii. Na hicho ndicho kinachompa furaha Augustin Nyabutsitsi, mwalimu mwenye umri wa miaka 74 aliyemfundisha Rais wa Rwanda, Paul Kagame katika madarasa ya sita na saba kati ya mwaka 1967 na 1968. Nyabutsitsi ambaye bado ni mwalimu, akifundisha katika Shule ya Le Bon Berger iliyopo Kimironko, Kigali, anakiri kwamba alimwadhibu Kagame wakati anasoma Shule ya Msingi Rwengoro iliyopo katika kambi ya wakimbizi Gahunge nchini Uganda.
Kwa mujibu wa mwandishi Marie-Anne Dushimana wa gazeti la Newtimes la Rwanda, ikiwa imepita miaka 50 sasa, mwalimu huyo anasema anawakumbuka vyema wanafunzi wake wa miaka hiyo. “Kagame alikuwa kama watoto wengine, lakini alikuwa na utofauti, alikuwa mwerevu sana. Alipendelea masomo ya Hisabati na Kiingereza. Alikuwa pia mdadisi, hakuacha kuuliza maswali mpaka alipoona amejiridhisha,” anasema Nyabutsitsi na kuongeza kuwa, daima Kagame alikuwa kinara darasani kwake.
Aidha, anakumbuka kuwa enzi hizo, Kagame alipendelea mno mchezo wa soka, akitumia mpira wa `chandimu’ uliotengenezwa na kufungwa kwa kamba za majani ya mgomba. Nyabutsitsi anasema hakuna kitu kinachofurahisha kwa mwalimu, kama kuona mwanafunzi wake anamkumbuka na kutambua mchango wa mwalimu katika maisha. Anasema kwa miaka mingi alikuwa na ndoto za kuonana na mwanafunzi wake, Kagame, bila ya kujua kuwa Rais huyo wa sasa wa Rwanda pia alikuwa na ndoto kama hizo.
Alisema hali hiyo siku alipokutana na Rais Kagame mkutanoni huko Nyagatare, ambako aliuliza kama kuna yeyote anayefahamu anakoishi mwalimu wake wa shule ya msingi, Augustin Nyabutsitsi. Alimkabidhi pia jukumu hilo Profesa Manasseh Nshuti, akimtaka ahakikishe anamtafuta Mwalimu Nyabutsitsi. Hatimaye, Kagame na mwalimu wake walikutana Januari 25, mwaka 2016.
Kwa sasa, Nyabutsitsi anaishi eneo la Kata ya Kinyinya katika wilaya ya Gasabo katika kijiji cha kisasa maarufu kama “Kwa Dubai”. Anaishi katika nyumba ya kisasa ya vyumba vinne aliyozawadiwa na Rais Kagame. “Tulipokutana, sikuomba chochote kutoka kwake, lakini nilishangaa alikuwa na taarifa nyingi juu yangu. Aliniambia amesikia naishi nyumba ya kupanga, akaagiza nipatiwe nyumba ya kisasa. Hiki ndicho unachokiona (anaonesha nyumba), ni zawadi ya Rais Kagame. Sikuwa na ndoto za kumiliki nyumba ya aina hii.
Namshukuru sana,” alisema Nyabutsitsi huku sura yake ikiwa na tabasamu pana. Anasema tukio hilo liliwashitua wengi, kiasi cha kumiminika kuishuhudia. Dada wa Nyabutsitsi, Teddy Kawera (60) ambaye pia ni Mwalimu katika shule ya Wellspring Academy ya jijini Kigali, anasema kwa ujumla, zawadi hiyo ya nyumba ikiwa sawa na miujiza kwao.
“Tulikuwa tunaishi nyumba ya vyumba vitatu ya kupanga eneo la Kanombe kwa gharama ya Faranga za Rwanda 150,000. Kodi ya nyumba sasa imebaki historia, tunaishi kwa amani, bila ya kuumiza kichwa kufikiria kodi ya pango, asante Rais Kagame,” anasema Kawera. Furaha ya Mwalimu Anasema amekuwa mwenye furaha mno kuona baadhi ya wanafunzi wake wamekuwa watu mashuhuri nchini Rwanda.
“Naamini nimekuwa na faida kwa nchi yangu. Kuna maofisa wengi wakubwa na wanajeshi niliowafundisha, miongoni mwao ni Joseph Mugambage anayefanya kazi na Rais Kagame, pia wamo Meja Rugira, Alexis Kagame na wengine wengi. Orodha ni ndefu, lakini kinara wao ni Rais Kagame,” anasema Nyabutsitsi. Akiwa katika fani ya ualimu kwa miaka 50 sasa, Mwalimu Nyabutsitsi anasema siku zote amekuwa na wito wa kufundisha watoto wa Rwanda. “Hakuna kinachonifurahisha kama kuona watu niliowafundisha wanageuka kuwa muhimu katika nchini… ni bahati iliyoje,” anasema.
Anasema mazingira ya kazi ya walimu, si kigezo cha kushindwa kufundisha vyema, bali kiu ya kufanya kazi inapaswa kuwa mbele, ikiwa ni pamoja na kuwa na upendo kwa wanafunzi. “Nashauri walimu wasiangalie mazingira ya kazi tu, bali mwito kwanza. Wanafunzi wakiona wanapendwa, hurudisha upendo kwa walimu wao na hata kuendeleza upendo kwa wengine.
Zawadi hii ya nyumba ni uthibitisho wa haya niyasemayo, nimefarijika kukumbukwa na mwanafunzi wangu ambaye kwa sasa ni Rais wa Rwanda, Paul Kagame,” anasema. Stevenson Mutunzi, mwalimu wa Shule ya Le Bon Berger, anasema amepata fundisho kubwa kutoka kwa Mwalimu Nyabutsitsi. “Ametupa fundisho kubwa la uvumilivu na kuipenda kazi licha ya changamoto kadhaa zikiwemo za mishahara,” anasema.
Naye Egide Musoni, Mjumbe wa Kamati ya Wazazi wa shule ya Le Bon Berger, anasema amefurahi kuona watoto wao wakifundishwa na mwalimu aliyemfundisha pia mtu mashuhuri kama Rais Kagame. Baada ya kushuhudia mabadiliko makubwa ambayo Rwanda imeyafikia kimaendeleo tangu mwaka 1994, anaamini miaka michache ijayo nchi hiyo chini ya Rais Kagame itapiga hatua zaidi na zaidi, hivyo anamwombea maisha marefu `mwanafunzi’ wake.
CHANZO HABARI LEO

Posted by Editor on 14:24. Filed under , , . You can follow any responses to this entry through the RSS 2.0

0 comments for MWALIMU WA RAIS KAGAME MSINGI BADO ASHIKA CHAKI

Post a Comment

Recent Entries

Recent Comments

Photo Gallery